Nina shauku kubwa kuhusu Haki za Binadamu

Get monthly
e-newsletter

Nina shauku kubwa kuhusu Haki za Binadamu

— Okwa Morphy kutoka Nijeria, nahudumu Sudan Kusini
15 May 2020
-Okwa Morphy from Nigeria, serving in South Sudan
-Okwa Morphy from Nigeria, serving in South Sudan
Okwa Morphy kutoka Nijeria, nahudumu Sudan Kusini

Tufahamishe kidogo kukuhusu?

Naitwa Okwa Morphy kutoka Nijeria, nahudumu Sudan Kusini. Mimi ni mfanyakazi wa Kujitolea wa Umoja wa Mataifa (UNV) na Misheni ya Umoja wa Mataifa huko Sudani Kusini (UNMISS). Umri wangu ni miaka 49 na nina shahada ya uzamili katika uanasheria. Uwanja wangu wa utaalamu ni haki za binadamu.

Unafanyia kazi wapi?

Kwa sasa niko Yambio, mji mkuu wa Jimbo la Ikweta, Sudan Kusini. Nafanya kazi na jamii ya mashinani na wadau wengine kuhamasisha kuhusu umuhimu wa kuimarisha na kulinda haki za kimsingi za binadamu na utu kwa wote, hasa wanawake na watoto. Napenda ninachokifanya!

Je, majukumu yako katika misheni ni yapi na siku yako ya kawaida huwa vipi?

Kama Afisa wa Haki za Binadamu na UNMISS, majukumu yangu ya msingi ni pamoja na kufuatilia, kuchunguza, kuorodhesha na kuripoti juu ya ukiukwaji wa haki za binadamu.

Hii ni kazi nyeti na ngumu ambayo kwa pamoja inajumuisha kufuatilia pande zote zinazozozana na jinsi matendo yao (au kutotenda) yanavyoathiri haki za raia.

Siku ya kawaida kwangu huku Yambio inajumuisha kufika ofisini mapema ili kutafuta masasisho kutoka kwa makao makuu ya misheni huko Juba, kisha kuanza safari ya kukutana na washiriki wa ndani. Kila mara natembelea vituo vya wafungwa kwa madhumuni ya ufuatiliaji. Sehemu ngumu zaidi ya siku yangu ni wakati wa kutembelea vitengo maalum vya ulinzi vya hospitali za mitaa ili kufuatilia na kurekodi visa vilivyoripotiwa vya dhuluma za kijinsia dhidi ya wanawake, ambavyo kwa bahati mbaya ni kawaida Sudan Kusini.

Je, umekuwa mfanyakazi wa kujitolea wa Umoja wa Mataifa kuanzia lini na ilikuwaje ukawa mmoja?

Nilijiunga na UNMISS kama mfanyakazi wa kujitolea wa Umoja wa Mataifa mnamo Agosti 2017. Hii ndiyo misheni yangu ya kwanza. Niligundua wavuti ya Wafanyakazi wa Kujitolea wa Umoja wa Mataifa kwa bahati tu nilipokuwa nikitumia mtandao nchini Nijeria siku moja. Wavuti ulivutia makini yangu mara moja na nikahimiza wataalamu wengine wajitolee kwa Shirika la Umoja wa Mataifa. Nilituma maombi na nilifurahia wakati miezi mitatu baadaye nilipopata majibu ya kuhudumu nchini Sudan Kusini. Ilikuwa ndoto yangu imetimia kikazi, kwani ilikuwa fursa ya kufanya kazi ninayopenda sana na katika ngazi ya kimataifa.

Je, familia yako na marafiki nyumbani walifikiria nini kuhusu uamuzi wako wa kuondoka nchini mwako na kufanya kazi ya misheni ya Umoja wa Mataifa ya kulinda amani?

Mama yangu alitatizika sana mwanzoni na hakuelewa ni kwa nini nilitaka kuacha utulivu wa nyumbani kwenda misheni ya nyanjani katika nchi ambayo ilikuwa na mzozo ulioendelea, umaskini na njaa kali. Lakini ndugu zangu walikuwa wananiunga mkono zaidi kwa sababu walihisi ni fursa ya kipekee, lazima nikubali, ilichukua kazi kubwa kumshawishi mama yangu aweze kukubali. Hata hivyo, ninafurahi kusema kwamba kadri wakati ulivyozidi kwenda na kuanza kutekeleza majukumu yangu, familia yangu inajivunia sana.

Je, kwa muhtasari, ni mambo gani muhimu yametokea katika misheni yako ya sasa ya kulinda amani:

Kwa muhtasari tajriba yangu katika UNMISS bila shaka imenipa fursa ambayo ninahitaji kuangazia ukiukwaji wa haki za binadamu na sheria za kibinadamu. Inaweza kuwa changamoto, na hata kuhofisha wakati mwingine. Lakini ninahisi kuwa kwa kiasi kidogo, ninahakikisha kuwa dhuluma ambazo zimepatikana dhidi ya raia na watu walioko hatarini, hususani wanawake na watoto, hatimaye zitashughulikiwa. Kwa njia fulani, naweza kusema nimechangia katika mfumo wa haki na uwajibikaji, na pia mchakato wa uponyaji kwa Sudan Kusini.

Je, ni vitu gani vitatu unavyopenda zaidi kuhusu misheni hii na nchi unayoitumikia?

Tajriba yangu mjini Yambio imenifundisha kuacha mapendeleo yangu ya kibinafsi, niwe huru kujifunza kutoka kwa wenzangu. Imenisaidia sana na kunifanya niwe mtu bora na mtaalamu mzuri. Ninashukuru sana kwa tajriba hii katika UNMISS kwa sababu imenifundisha umuhimu wa uvumilivu na kuniwezesha kupanua stadi zangu sana.

Ninachopenda kuhusu Sudan Kusini ni watu wanaokaribisha sana na wakarimu. Licha ya changamoto zote wanazokumbana nazo kila siku - ugumu wa kulisha watoto wao, kupata riziki, kulinda nyumba zao na familia - unaweza kuhisi upendo wao unapokutana nao. Licha ya yote waliyoyapitia kama watu na nchi, tabasamu kwenye nyuso zao zimejaa matumaini. Kwangu, uvumilivu huu katika shida kama hizi ni nadra.

Je, ni sehemu gani ya kazi yako ambayo ina changamoto zaidi?

Ninachochewa ninapozungumza na watu ambao haki zao za kibinadamu zimekiukwa kwa njia fulani, au wale ambao wamepitia dhuluma ya kingono. Ninaona kiwewe machoni mwao nikisikia sauti zao. Daima imekuwa ni sehemu ngumu sana ya kazi yangu.

Je, unafikiri walinda amani wa kike hutumika kama vielelezo bora kwa watu wa eneo hilo?

Hakika! Nadhani tunawapa wanawake na wasichana uwezo bora wa kutamani. Nikiwa miongoni mwa jamii za huko Ikweta ya Magharibi wanawake wengi huja kwangu na kuniambia kuwa wanatarajia binti zao watakuwa kama mimi siku moja. Huwa nawaambia kuwa binti zao wanaweza kuwa kama mimi wakipewa fursa ya kwenda shule na kukamilisha masomo yao. Kwa jumla, walinda amani wa kike kutoka UNMISS wanapendwa na wanaheshimiwa miongoni mwa jamii za wenyeji.

Je, ungesema nini kwa vijana wanaowazia kufanya kazi ya kulinda amani?

Kulinda amani sio kazi ya watu walio na moyo dhaifu. Inaleta ubinadamu wetu sote na inahusu kutumikia jamii na watu wanaohitaji msaada wako zaidi. Kwa hivyo, ikiwa kweli unataka maisha yawajibikie kitu kikubwa kuliko wewe mwenyewe, ninakuhimiza sana kuzingatia kazi ya kulinda amani. Sio rahisi kila wakati kuwa mbali na familia na wapendwa wako na hali ya kazi inaweza kuwa ngumu; lakini kujitolea hatimaye kunafaa!