Ãå±±½ûµØ

Kulisha Afrika kutoka Afrika: Wakulima wadogo kupigwa jeki na AfCFTA

Get monthly
e-newsletter

Kulisha Afrika kutoka Afrika: Wakulima wadogo kupigwa jeki na AfCFTA

Athari ya COVID-19 imefichua udhaifu wa mifumo ya sasa ya chakula, lakini pia imefunua fursa kwa Afrika kufanya biashara na Afrika chini ya AfCFTA
Busani Bafana
Afrika Upya: 
10 June 2021
Mkulima
FAO/Sebastian Liste
Wakulima kutoka Ushirika wa Mboga ya Wanawake wa Koinadugu, wakivuna kabichi.

Senamiso Ndlovu mwenye miaka 32, ni mkulima mdogo mwenye ndoto kubwa ya uzalishaji wa chakula. Mbegu ya matarajio yake ya kilimo ni mahitaji ya chakula mijini. Ameimarisha uzalishaji wa pilipili hoho, mboga ya malenge, nyanya na matango ili kukidhi mahitaji ya mazao mabichi mjini Bulawayo, mji mkubwa nchini Zimbabwe.

Bi Ndlovu, anayesimamia shamba la familia huku akisomea shahada ya Uzamili katika Biashara ya Kilimo, anasema anafurahia kuulisha mji, lakini anataka sehemu ya soko la chakula la Afrika. Eneo la Biashara Huru la Bara la Afrika (AfCFTA) lililozinduliwa hivi karibuni linaweza kuwa soko analolihitaji.

"Kwa mfano natamani kuuza mazao yangu nchini Kenya, ambalo ni soko lenye ushindani, na ninathamini soko kubwa barani Afrika," anaeleza Bi Ndlovu.

Kwa Bi Ndlovu, soko la kuuza barani Afrika ni matarajio ya kufurahisha katika kukuza biashara yake ya kilimo na kujifunza maoni mapya ya biashara.

Kuingia katika soko la ndani kumekuwa jambo ngumu. Amelazimika kukopa pesa kwa riba ya juu ili kuongeza mara tatu uzalishaji wake wa sasa kufikia maagizo makubwa na kuinua viwango vya ubora.

Kuuzia ulimwengu hata ni ngumu zaidi; kuna kizuizi kikubwa katika kupata idhini ya kusafirisha bidhaa nje, kukidhi masharti magumu ya kuzuia kuenea kwa wadudu na dhamana ya usambazaji, bila kutaja fedha zinazohitajika kabla ya uzalishaji. Kuuzia Afrika kutabadilisha masuala ya chakula, anasema.

"Wakulima wadogo wanahitaji kuwa katika muungano wakati huu ili kuweza kujumlisha mazao yao ili kuyauzia masoko ya nje," anaeleza Bi Ndlovu.

Mipaka wazi, chakula zaidi,Ìý pesa zaidi

Kilimo kinachangia karibu asilimia 30 ya Pato la Taifa la bara, kulingana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).

Athari za COVID-19 zimefunua udhaifu wa mifumo ya sasa ya chakula huku mataifa yakifunga mipaka wakati wa masharti ya kutotoka nje, yakizuia uagizaji na usafirishaji wa chakula lakini ikifunua wazi fursa ya Afrika kufanya biashara na Afrika chini ya masharti ya biashara ya upendeleo.

Kupitia AfCFTA, muungano wa kibiashara wa kukabiliana na upungufu wa biashara na ukosefu wa ajira ulizinduliwa. Muungano huu unaahidi kuwafanya Waafrika wengi kununua, kula na kuvaa bidhaa na huduma za 'zilizotengenezwa Afrika' kwa gharama nafuu.

Kilimo cha Afrika - kimekumbwa na uzalishaji duni, utunzaji mbovu wa kiufundi, uwekezaji usiopangwa na sera inayohitilafiana - kinaweza kugeuzwa kwa kuboresha biashara miongoni mwa mataifa 55 wanachama wa Umoja wa Afrika.

Kuirejeshea Afrika Hadhi yake

Kilimo kinachostawi kinarejesha hadhi ya Afrika, anasema Profesa Lindiwe Majele Sibanda, mtetezi wa usalama wa chakula na Mkurugenzi wa Kituo cha Muungano wa Vyuo Vikuu vya Utafiti vya Afrika katika Mifumo ya Chakula Endelevu katika Chuo Kikuu cha Pretoria, Afrika Kusini.

Afrika inaagiza chakula cha zaidi ya dola bilioni 50, kingi kutoka nje ya bara. AfCFTA imetekeleza malengo ya viwango na biashara, yanayofanana na mfumo wa upendeleo kwa Afrika.

"Tumeeleza chakula kwa upana, na tunaweza kuanza na kile tunachoweza kuzalisha kwa njia bora kwa mazingiraÌý na uendelevu," Profesa Sibanda aliambia Afrika Upya, akisisitiza kuwa kuweka upendeleo wa biashara unapaswa kutumiwa kama kichocheo cha ushindani wa ndani na upendeleo kwa nchi za Kiafrika.

"Kisababishi kikuu cha gharama kubwa ya uagizaji wa chakula barani Afrika kimekuwa sera mbovu ambazo haziwainui wakulima na kuchochea uzalishaji wa ndani," Profesa Sibanda asema.

Nchini Nijeria, imekuwa bei rahisi kuagiza mchuzi wa nyanya kuliko kuuzalisha nchini, huku huko Zimbabwe ni rahisi sana kuagiza maziwa kuliko kuzalisha nchini.

Prof. Sibanda anahimiza serikali kukagua na kutathmini gharama za uzalishaji wakati wa kutambua faida za upendeleo kwa Afrika.

"Afrika tunayotaka ni Afrika inayoleta heshima kwa Waafrika," Profesa Sibanda alisema, akiongeza kuwa hakuna njia bora ya kurejesha heshima kuliko kupitia AfCFTA ambayo hailengi kuleta ukiritimba kwa biashara bali kulidhihirishia Shirika la Biashara Duniani kwamba Afrika inaweza kujadili mikataba kwa faida yake kwa sauti moja.

Kilimo kinahitaji fedha ili kukua

Uwekezaji wa kipekee katika pembejeo zilizoboreshwa, umwagiliaji maji, uhifadhi na miundombinu ya kimsingi itasukuma mbele ukuaji wa kilimo barani Afrika, McKinsey na Wengine wanaeleza, wakitoa wito wa kuboreshwa kwa ushindani wa bara zima, sio tu mavuno. Kuongezeka kwa miji na kuongezeka kwa watumiaji wa tabaka la kati kunatabiriwa kusaidia kuzalisha dola 645 kwa matumizi ifikapo mwaka 2025 katika mazao mabichi, maziwa, nyama, chakula kilicho tayari na vinywaji.

Sekta ya kibinafsi lazima itafute mbinu za kunufaika kutokana na uwezo wa kilimo wa Afrika kwa kutatua changamoto za usambazaji wa chakula kupitia kuwezesha masharti rahisi ya malipo kwa wafanyabiashara wa kilimo ili kuboresha ununuzi wa pembejeo. McKinsey anapendekeza ukuzaji wa ushirikiano ili kupunguza hatari ya kukosa kulipa.

Kwa mfano, Muungano wa Afrika wa Mbolea na Kilimobiashara (AFAP) umetoa dhamana ya upotezaji wa kwanza kwa wauzaji wa mbolea ili kusongesha masharti ya malipo kwa wafanyabiashara wa kilimo nchini Tanzania, na kuchangia ongezeko la takriban asilimia 35 ya mauzo ya mbolea.

Kutumia teknolojia na kuleta ubunifu

Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la Mapinduzi ya Kijani Afrika (AGRF) Debisi Araba anaiambia Afrika Upya kwamba teknolojia na mifumo inayoboresha ufanisi wa usafirishaji wa bidhaa na usambazaji wa habari na shughuli za kubadilisha ni matarajio ya kufurahisha kwa Afrika.Ìý

Biashara zinazoanzishwa kama Lori Systems na Kobo360 zinatumia data nyingi na uchanganuzi wa habari ili kuboresha ufanisi wa sekta ya usafirishaji, mahitaji ya uainisho na kuwaunganisha na huduma zinazohitajika za usambazaji, Bwana Araba anasema.

Bwana Kanayo Nwanze, CGIAR Mwakilishi Maalum wa Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mifumo ya Chakula, anaamini Afrika haikuwa mwagizaji wa chakula kwa sababu kilimo chake kilichangia zaidi ya asimila 60 ya Pato la Taifa kabla ya miaka ya themanini.

Hivi leo, Afrika ni mwagizaji wa chakula baada ya kukosa kuekeza katika kilimo na viwanda vinavyotumia mafuta ya madini, Bwana Nwanze anaeleza.